KATIKA hatua inayolenga kukuza biashara na mahusiano kati ya Tanzania na Kenya‚ kampuni ya Skyward Airlines imezindua rasmi shughuli zake Jijini Dar es Salaam. Akizungumza na waandishi wa habari‚ Meneja Mkuu wa Skyward Airlines‚ Diana Nyambura alisema wamekuja kuleta mageuzi katika sekta ya anga katika nchi hizi mbili na nyinginezo.
“Tumekuja na mambo ya kusisimua na ya aina yake kama vile unafuu wa nauli‚ utendaji bora na kujali muda ili kuwapa wateja wetu mambo ambayo walikuwa wanayatamani kwa muda mrefu‚”
alisema.
Katika mkutano huo‚ Skyward ilitangaza safari mpya ya Dar es Salaam-Nairobi kila siku huku ndege zao zikipita Mombasa‚ Kenya siku za Alhamisi na Jumamosi. Safari ya Dar es Salaam na Mombasa zitakuwa ni nusu saa tu.
Alisema Tanzania na Kenya zimekuwa zikitegemeana kwa muda mrefu kibiashara kwa maana hiyo wakaona umuhimu wa kuja na usafiri wa anga ambao ni nafuu ambao utarahisisha watu kusafiri kwa haraka. alisema.
“Nauli itakuwa ya nafuu kabisa ili kuwezesha watu wengi zaidi kusafiri kwa ndege kutoka Nairobi-Dar es Salaam na Dar es Salaam Nairobi na Mombasa. Tutatangaza nauli hizi mara baada ya promosheni yetu kumalizika‚”
alisema.
Kwa mujibu wa Meneja huyo‚ shirika hilo la ndege lina ndege za kutosha ili kuhakikisha hakutakuwa na ucheleweshaji wa aina yoyote kwa abiria.
“Moja ya sababu za watu kuchagua kusafiri kwa ndege ni ili waokoe muda na sisi kama Skyward tutahakikisha hakuna ucheleweshaji ili tulete utofauti katika soko. Hili linawezekana kabisa‚”
aliahidi.
Aliendelea kusema kuwa ili kuhakikisha wanapatikana wasafiri wengi wanaokuja Dar es Salaam na maeneo mengine ya Tanzania‚ kitengo chao cha masoko kiko makini kuhakikisha abiria wanapata taarifa zinazohitajika ili kuwasaidia abiria kufanya maamuzi.
“Tuna pia majarida mbalimbali katika ndege zetu ambayo yana matangazo ya vivutio vya kitalii na huduma nyingine zikiwemo za malazi. Tuna wahudumu wa ndege waliobobea na watawasaidia abiria kufanya maamuzi sahihi endapo watawauliza maswali wakati wako angani‚”
aliongeza.
Alisema shirika hilo liko makini katika suala la ajira kwa Watanzania kwani tayari wana ofisi katika jengo la Viva Jijini Dar es Salaam.
Na Joyce Kasiki‚ Dodoma
Source: Times Majira